Saturday, July 14, 2012

TAARIFA ZILIZOINGIA:MKURUGENZI WA TANESCO ASIMAMISHWA KAZI

 MKURUGENZI Mtendaji wa Tanesco Amesimamishwa na Bodi ya wakurugenzi wa Shirika hilo ili kupisha Tuhuma zinazomkabili kuhusu ubadhilifu wa shirika na matumizi mabaya ya ofisi.Uchunguzi huo utafanywa na mchunguzi huru.Pamoja naye ameondolewa na wenzie kama mkuu wa fedha wa shirika na mkuu wa manunuzi ....Tutaendelea kuwapa taarifa zaidi

Wednesday, July 4, 2012

Mwl Christopher Mwakasege mnamo tarehe 17-19 August 2012 anatarajia kuwa mnenaji katika Summer Conference 2012 itakayoyanyika nchini UINGEREZA jimbo la MILTON KEYNES,Kongamano hili limeandaliwa na umoja wa watanzania wakristo waishio katika bala la Ulaya(CITE).

Kwa mujibu wa mmoja wa viongozi wa CITE Mch Emmanuel Chatawe, CITE SUMMER CONFERENCE 2012 itafanyika katika ukumbi wa


Oakgrove Leisure centre Brickhill Street Middleton Milton Keynes MK10 9JQ
17/08/2012 Time 2:00pm-9pm
18/08/2012 Time 10am-9pm
19/08/2012 Time 11am-7am


Kwa mawasiliano zaidi

Rev. Chatawe 07944632826 ,
Pas. Kimani 07522050673,
Sis Jane 07522302935 au
Sis. Flora 07916160641

Chakula cha mchana kitatolewa Jumamosi na Jumapili kwa wote watakaohitaji kwa Paund 3(£3.00).Wote mnakaribishwa

Monday, July 2, 2012







Mbunge wa Jimbo la Ubungo (Chadema), John Mnyika.
LEO tarehe 1 Julai 2012 kumesambazwa katika mitandao ya kijamii na baadhi ya vyombo vya habari hotuba ya Mh. Dkt. Jakaya Kikwete Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa wananchi inayotajwa kutolewa tarehe 30 Juni 2012.
Kufuatia hotuba hiyo na kufuatia mwito kutoka wachangiaji wa mitandao ya kijamii na baadhi ya vyombo vya habari kutaka maoni yangu kuhusu hotuba husika, naomba nichukue fursa hii kutoa maoni kwa nafasi yangu ya ubunge kuhusu hotuba tajwa kama ifuatavyo:
Hotuba hiyo ya Rais imeibua mjadala na masuala ambayo yanahitaji kujadiliwa bungeni katika mkutano wa nane wa Bunge unaoendelea hivyo, serikali isiendelee tena kutumia kisingizio cha mahakama kulizua bunge kujadili masuala husika wakati yenyewe inayajadili na kuyatolea maelezo na maelekezo pamoja na kuchukua hatua hususani kuhusu suala la mgomo wa madaktari.
Hotuba hiyo ya Rais ukindoa suala la usafirishaji haramu wa watu nchini inaelekea kuwa ndiyo kauli ya Serikali ambayo Waziri Mkuu Mizengo Pinda aliahidi kwamba ingetolewa bungeni lakini baadaye serikali ikasema haitatoa kauli. Uamuzi wa Serikali kuitoa kauli hiyo kupitia hotuba ya Rais una mwelekeo wa kukwepa wabunge wasijadili hotuba husika na pia wasitimize wajibu wa kikatiba wa ibara 63 (2) wa kuisimamia serikali kwa niaba ya wananchi.
Hivyo, Ofisi ya Rais na Ikulu wanapaswa kutoa maelezo kwa umma sababu za Rais kutolihutubia taifa tarehe 30 Juni 2012 kama ilivyotangazwa katika baadhi ya vyombo vya habari vya kielectroniki na badala yake hotuba ya Rais kusambazwa tarehe 1 Julai 2012 kupitia mitandao ya kijamii na baadhi ya vyombo vya habari na iwapo masuala ya hotuba hiyo kuhusu mgomo wa madaktari ndiyo yale ambayo Waziri Mkuu Mizengo Pinda alikusudia kuyaeleza bungeni.
Aidha, kwa kuwa bunge litajadili mapitio ya utekelezaji wa bajeti ya Ofisi ya Rais kwa mwaka wa fedha 2011/2012 na makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2012/2013 kuanzia kesho tarehe 2 Julai 2012 na kuendelea ni muhimu wabunge wakajadili pia masuala ambayo Rais ameyaeleza kwa taifa na kutimiza wajibu wa kikatiba kwa mujibu wa ibara ya 63 (2) wa kuishauri na kuisimamia serikali.
Kuhusu Usafirishaji Haramu wa Binadamu Nchini
Ni vizuri hotuba ya Rais imeeleza wazi kwamba tukio la Chitego, Dodoma la wahamiaji haramu kukamatwa na wengine kukutwa wamekufa si la kwanza kutokea hapa Tanzania kwa kuwa kwa kipindi cha miaka kumi kumekuwa na ongezeko la usafirishaji haramu wa binadamu katika taifa letu kupitia mipaka ya mikoa mbalimbali hapa nchini. Kwa mbinu yoyote ile ambayo imetumika, matukio haya yanaashiria kwamba mipaka yetu haipo salama kwa kuwa kama malori na vyombo vingine vya usafiri vyenye watu wasio na hati za kuingilia nchini wanaweza kuingia kwa wingi kwa nyakati mbalimbali tafsiri yake ni kwamba nchi iko kwenye hatari ya kuingiziwa pia vitu vingine haramu ikiwemo madawa ya kulevya na silaha hali ambayo ni tishio kwa usalama wa nchi na maisha ya wananchi. Ni vizuri Rais amekutana tarehe 27 Juni 2012 na wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama kuzungumzia tukio hilo; hata hivyo, zaidi ya kuwapongeza vyombo vya dola kwa kazi nzuri ya kudhibiti shughuli za biashara haramu, nilitarajia kwamba Rais kwa mujibu wa mamlaka yake ya ibara ya 33 (2) ya mkuu wa nchi, kiongozi wa serikali na amiri jeshi mkuu angeagiza uchunguzi ufanyike kuhusu udhaifu uliojitokeza na kuagiza hatua kuchukuliwa kwa walishindwa kudhibiti hali hiyo katika mipaka ambayo biashara haramu ya usafirishaji wa watu inapitia. Izingatiwe kwamba mianya hii katika mipaka yetu ina athari pana sio katika suala hili tu bali pia katika usalama wa maisha ya wananchi kama ilivyo katika mikoa ya Kigoma, Kagera na kwingineko ambapo uhai wa wananchi na mali zao uko mashakani kutokana na uvamizi toka kwa wahamiaji haramu. Aidha, athari za hali hiyo zimejitokeza katika usambazaji wa chakula toka kwenye hifadhi ya taifa ambapo pamoja na Serikali kutumia zaidi ya bilioni 27 kusambaza mahindi na nafaka nyinginezo bei za bidhaa hizo katika Soko la Dar es salaam ikiwemo katika Jimbo la Ubungo hazikushuka kutokana na vyakula hivyo kutoroshwa na kuuzwa nje ya nchi kutokana na udhaifu katika ulinzi kwenye mipaka.
Hivyo, ni muhimu wabunge wakati wa mjadala wa bajeti ya ofisi ya Rais wataka kuongezeka kwa uwajibikaji na usimamizi wa utawala wa sheria ili kudumisha amani nchini.
Hatua ambazo zinapaswa kuchukuliwa ni pamoja na bunge kuisimamia serikali kuhakikisha idara ya usalama wa taifa inafanya kazi kwa ufanisi zaidi katika kuvisaidia vyombo vingine vya dola kulinda mipaka ya nchi na pia matatizo ya maslahi katika vyombo vya ulinzi na usalama yanatatuliwa ili vyombo husika viweze kufanya kazi bila baadhi ya maofisa wake kujihusisha na vitendo vya ufisadi na kuruhusu biashara haramu za aina mbalimbali.
Kuhusu Mgomo wa Madaktari
Kuhusu mgomo wa Madaktari unaoendelea nchini hivi sasa; hotuba ya Rais imeendeleza kauli za upande mmoja ambazo zimekuwa zikitolewa na serikali kuhusu mgogoro huo bila taifa kupewa fursa ya kupata maelezo na vielezo vya upande wa pili; hivyo kuwa serikali imetoa kauli yake hadharani badala ya bungeni au mahakamani, ni muhimu pia taarifa ya kamati ya bunge ya huduma za jamii iliyoshughulia suala hilo na kukutana na pande zote mbili itoe taarifa yake bungeni na kwa umma.
Katika hotuba yake Rais amewaeleza kwa kiwango kikubwa wananchi namna ambavyo madaktari wanasababisha mahangaiko kwa wagonjwa wengi na kusababisha vifo kwa wengine lakini hakueleza kabisa mchango wa serikali katika kusababisha hali hiyo. Hivyo, kwa kuwa pande zote mbili zinachangia katika athari zinazoikumba nchi na wananchi kutokana na mgomo; ni muhimu chombo cha tatu kikaingilia kati kuwezesha ufumbuzi kupatikana na chombo hicho ni bunge ambalo ndilo lenye wajibu wa kuisimamia serikali. Jitihada za kuwalazimisha madaktari kurejea kazini bila majadiliano ya pande mbili mbele ya chombo cha kuisimamia serikali kushughulikia chanzo cha mgogoro huo zinaweza kuleta ufumbuzi wa muda mfupi na athari za muda mrefu.
Ieleweke kwamba hata madaktari wakisitisha mgomo wa wazi kutokana na amri ya mahakama na agizo la Rais, migogoro katika ya serikali na watumishi wa umma wenye kusababisha migomo baridi ya chinichini ina madhara ya muda mrefu kwa taifa.
Mathalani, kutokana na migomo baridi na huduma mbovu katika sekta ya afya wananchi wa kawaida wamekuwa wakifa kutokana na magonjwa yanayotibika.
Migomo ya chini kwa chini ya walimu na mazingira mabovu yamekuwa yakisababisha kudidimia kwa elimu katika shule za umma; mwanafunzi aliyehitimu masomo yake bila kujua kusoma na kuandika hana tofauti na mgonjwa anayekufa kwa kukosa huduma.
Hali hii ya kugoma kusiko kwa wazi imeenza kujipenyeza mpaka kwa askari wa vyombo vya ulinzi na usalama kwa kuachia mianya ufisadi na kushindwa kusimamia utawala wa sheria kama ivyodhihirika kwa kuongezeka kwa vitendo vya biashara haramu katika taifa letu.
Rais amewaeleza wananchi kuwa kati ya tarehe 10 Aprili, 2012 na tarehe 30 Mei, 2012, vilifanyika vikao sita vya majadiliano kati ya Serikali na Chama cha Madaktari na kwamba katika mazungumzo hayo hoja au madai 12 ya madaktari yalizungumzwa na pande zote mbili zilifikia muafaka na kukubaliana wa pamoja kwa mambo saba. Hata hivyo, katika masuala matano yaliyobaki, Rais hakueleza kwa wananchi nini ambacho serikali ilikuwa tayari kutoa kwa kila madai na kwa kiasi gani badala yake ameonyesha tu kwa ujumla kwamba madai hayo hayatekelezi.
Aidha, kufuatia hotuba hii ya Rais Madaktari nao wana wajibu wa kuueleza umma msingi wa madai yao na kwa kiwango gani walikuwa tayari kushuka kutoka katika madai yao ya awali, kinyume na hayo itaonekana kwamba madaktari waliingia katika majadiliano wakiwa na msimamo wa kutaka madai yao pekee ndiyo yakubaliwe wakati ufumbuzi wa mgogoro wa pande mbili hupatikana kwa win win (give and take).
Ni vizuri ikafahamika kwamba katika majadiliano, pande zote mbili huwa na mapendekezo yake; hivyo upo uwezekano kwamba yapo madai ambayo madaktari wameyatoa ambayo serikali haina uwezo wa kuyatimiza kwa kiwango walivyopendekeza na yapo ambayo serikali imeyakataa wakati ambao ina uwezo wa kuyatekeleza hata ikiwa kwa kiwango pungufu ya kile kilichopendekezwa na madaktari.
Suluhu katika mgogoro kama huo ambao kila upande una mapendekezo yake linapaswa kufanywa na vyombo vya usuluhishi; hata hivyo kuwa suala hili linahusu mgawanyo wa rasilimali za nchi na bajeti ya serikali, chombo chenye mamlaka ya kuisimamia serikali kwa niaba ya wananchi ni bunge.
Na kwa kuwa kamati ya bunge ya huduma za jamii ilikutana na pande mbili, ilikuwa muhimu kwa serikali kabla ya kupeleka shauri mahakamani kurejesha kwamba suala husika bungeni ambalo ndilo lenye wajibu wa kupendekeza vipaumbele vya mpango wa serikali na ndilo lenye kuidhinisha bajeti ya matumizi ya serikali.
Uamuzi wa serikali kukimbilia mahakamani kabla ya majadiliano ya bunge umechangia katika kusababisha mgomo wa madaktari, hivyo ushauri wangu kwa Rais Kikwete ni kwa serikali kufuta kesi iliyoko mahakamani ili bunge lipewe fursa ya kujadili ripoti yake kamati yake na kupitisha maazimio ya kuwezesha suluhu kati ya serikali na madaktari.
Mahakama iwe ni hatua ya mwisho baada ya mihimili miwili muhimu ya serikali na bunge kushindwa kuupatia ufumbuzi mgogoro unaoendelea wenye athari kwa nchi na maisha ya wananchi.
Rais Kikwete ameeleza taifa kwamba Serikali imeongeza sana bajeti ya sekta ya afya kutoka shilingi bilioni 300 2005/2006 hadi shilingi trilioni 1.2 mwaka 2011/12; hata hivyo serikali inapaswa pia kulieleza taifa namna ambavyo kiwango hicho cha fedha kinapungua ukiweka kizio (factor) cha kushuka kwa thamani ya shilingi na mfumumo wa bei ukilinganisha mwaka 2005 na 2012.
Ukweli ni kwamba bajeti ya Sekta ya Afya bado ni ndogo kwa kuwa serikali haijatimiza bado azimio la kutenga asilimia 15 kwa ajili ya bajeti ya afya pia, hata kiwango hicho cha ongezeko la fedha hakijaleta matokeo ya kutosha kutokana na matumizi kuelekezwa kwenye baadhi ya maeneo yasiyokuwa ya kipaumbele na kuwa na utegemezi wa kiwango kikubwa cha fedha za wahisani ambazo kwa mwaka huo wa 2011/2012 aliourejea Rais Kikwete hakikutolewa kwa kiwango kilichoahidiwa. Hivyo, Rais Kikwete awezeshe kuongezwa kwa fedha za ndani kwenye bajeti ya afya kwa mwaka wa fedha 2012/2013. Katika madai mengine Rais Kikwete ameeleza kwamba pande mbili zilifikia makubaliano nusu nusu, hali ambayo inaashiria kwamba madaktari wana hoja ambazo zinahitaji majadiliano hivyo, ni muhimu bunge likapewa nafasi ya kujadili kuweza kuwakilisha pande zote mbili za serikali na madaktari kuhusu nini kinawezekana na nini hakiwezekani ili kulinusuru taifa na mgogoro unaoendelea.
Rais Kikwete ametumia kwa kiwango kikubwa madai ya madaktari ya ongezeko la mshahara kujaribu kuwachonganisha wananchi na madaktari kwa kuwa na madai yasiyotekelezeka. Hata hivyo, ni muhimu ikafahamika kwamba sio madaktari pekee ambao wana mgogoro na mwajiri wao yaani serikali kuhusu kiwango cha mshahara bali pia watumishi wengine wa umma ikiwemo walimu.
Nyongeza iliyotolewa na serikali ya kati ya asilimia 15 na 20 kwenye mwaka wa fedha 2012/2013 ni tofauti na ahadi ambazo serikali imekuwa ikitoa kwa wafanyakazi za kuongeza mishahara na kupunguza kodi katika mishahara. Rais Kikwete na serikali warejee maoni na mapendekezo ya kambi rasmi ya upinzani kwa mwaka wa fedha 2011/2012 na 2012/2013 kuhusu nyongeza za mishahara kwa watumishi wa umma na vyanzo mbadala vya mapato vya kuongeza kwa ajili ya kuwa na uwezo wa kutimiza mahitaji. Uwiano wa sasa wa matumizi ya mishahara kuwa asilimia 48 ya bajeti badala ya uwiano mzuri wa asilimia 35 kuwa mishahara na na asilimia 65 zitumike kugharimia huduma na shughuli nyingine za maendeleo ya wananchi na taifa; ni matokeo ya udhaifu wa serikali katika kupanua vyanzo vya mapato, kupunguza matumizi ya kawaida yasiyo ya lazima na kuongeza fedha katika miradi ya maendeleo hali ambayo Rais Kikwete kuliwezesha bunge kuisimamia serikali na kuirekebisha.
Kuhusu Suala la Dkt. Steven Ulimboka
Rais Kikwete ameeleza wananchi kuwa ameelekeza vyombo vyetu vya ulinzi na usalama kufanya uchunguzi wa kina ili ukweli ujulikane; hata hivyo kauli hii inaashiria kukubaliana na hatua iliyochukuliwa na jeshi la polisi kuunda jopo la kuchunguza.
Nilitarajia Rais Kikwete kwa kutambua uwepo wa madai ya polisi kutuhumiwa kuhusika katika jaribio la mauji ya Dr Ulimboka angetangaza kuunda tume huru ya uchunguzi au walau angeongeza nguvu katika jopo la uchunguzi lililoundwa kwa kuunda timu ya maafisa waandamizi wa vyombo vya ulinzi na usalama na usalama pamoja na wadau wengine kutoka taasisi huru.
Rais Kikwete anapaswa kutumia madaraka yake kwa mujibu wa katiba kuunda tume huru ambayo inadhihirisha kwa vitendo kwamba watuhumiwa hawajichunguzi wenyewe na kuwezesha matokeo ya uchunguzi kuaminika.
Narudia kuwasihi madaktari kuendelea kuokoa maisha ya wananchi katika kipindi hiki kigumu lakini wakati huo huo Rais Kikwete aiongoze serikali kuepusha athari zaidi katika sekta ya afya ya kuwa na mgogoro na madaktari kwa kuliwezesha bunge kujadili suala hili na kulipatia ufumbuzi ikiwemo kupitia nyongeza ya bajeti ya Wizara ya Afya. Nimemwandikia barua Spika Anna Makinda akiwa ni mkuu bunge kama muhimili mmojawapo wa dola kuweza kuchukua hatua stahili, naomba pande zote zizingatie maoni yanayotolewa na wabunge kwa niaba ya wananchi kwa maslahi ya taifa.
Maoni haya yametolewa leo tarehe 1 Julai 2012 na:

Sunday, July 1, 2012




Rais Jakaya Mrisho Kikwete.
HOTUBA YA MHE. DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE,
RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA,
KWA WANANCHI, TAREHE 30 JUNI, 2012
Ndugu Wananchi, 
          Kama ilivyo ada naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehma, kwa kutujaalia uzima na kutuwezesha kumaliza nusu ya kwanza ya mwaka 2012 salama.  Kwa kutumia utaratibu wetu wa kuzungumza nanyi kila mwisho wa mwezi, leo napenda kuzungumzia mambo mawili. Jambo la kwanza ni suala la usafirishaji haramu wa binadamu nchini na la pili ni la mgomo wa madaktari.
Usafirishaji Haramu wa Binadamu Nchini
Ndugu Wananchi;
          Bila ya shaka mtakuwa mmezisikia taarifa za tukio la kushtusha na kuhuzunisha la kukutwa maiti 43 za watu wasiojulikana, zilizotupwa katika kichaka kilichopo kijiji cha Chitego, Wilayani Kongwa, Mkoa wa Dodoma tarehe 26 Juni, 2012.  Pamoja na maiti hao, walipatikana watu 84 wakiwa hai lakini wote wakiwa wamedhoofu na baadhi yao wakiwa mahututi.  Hatua za haraka zilichukuliwa kuwasafirisha watu hao hadi Dodoma ambapo wale waliokuwa mahututi walifikishwa Hospitali Kuu ya Mkoa wa Dodoma kwa matibabu na wengine walihifadhiwa katika Kituo cha Kati cha Polisi, Dodoma.  Maiti 22 zilipelekwa Dodoma na 21 zilipelekwa Morogoro kuhifadhiwa.
Taarifa zilizopatikana kutoka kwa wale walionusurika zimebainisha kuwa watu hao ni raia wa Ethiopia ambao walikuwa safarini kwenda Malawi na baadaye Afrika ya Kusini ambako wangetengenezewa utaratibu wa kwenda kuishi Marekani na Ulaya.  Kwa mujibu wa maelezo yao, safari yao ilianza miezi mitano iliyopita.  Mwezi mmoja waliutumia Ethiopia na miezi minne waliitumia Kenya kabla ya kuletwa Arusha ambako walipakiwa kwenye lori na kuanza safari ya kuelekea Malawi lakini ikaishia Chitego.  Lori walilopanda lilikuwa limezibwa kabisa na hivyo kusababisha vifo kwa kukosa hewa.
Tukio la Chitego, Dodoma la wahamiaji haramu kukamatwa na wengine kukutwa wamekufa si la kwanza kutokea hapa nchini.  Kwa jumla, katika kipindi cha takriban miaka 10 sasa kumekuwepo na tatizo kubwa la wahamiaji haramu kuingia nchini.  Kwa mfano, kati ya mwaka 2005 na hivi sasa jumla ya wahamiaji haramu 19,683 wamekamatwa.  Karibu wote wameshaondoshwa nchini na hivi sasa wapo karibu watu 1,500 tu magerezani wanaotumikia adhabu na kusubiri kurejeshwa makwao.  Wengi wa watu hao wanatoka Ethiopia na Somalia na baadhi kutoka Pakistan na Bangladesh.
Wahamiaji haramu wamekuwa wanaingia nchini kwa kupitia njia zisizo rasmi.  Wapo wanaotumia nchi kavu hasa kupitia mikoa ya Mara, Arusha, Kilimanjaro na Tanga.  Na, wapo wanaopitia baharini kwa kutumia fukwe za Pemba, Unguja na za mikoa ya ukanda wa Pwani ya Tanzania Bara yaani Tanga, Pwani, Lindi na Mtwara.
Ndugu Wananchi;
Kwa mujibu wa kauli zao, watu hao wamekuwa wanaeleza kuwa hawaji nchini kuhamia bali wao ni wapita njia tu.  Wanaelekea Afrika ya Kusini ambako wameahidiwa kuwa watatengenezewa mipango ya kuhamia Marekani na Ulaya.  Watu hao pia wamethibitisha kuwepo kwa watu maalum wanaojihusisha na usafiri wao tangu nchi watokako na zote wanazopitia mpaka kule waendako.  Aidha, wamesema kuwa wao wanawalipa watu hao ili wawasafirishe na hakika si kiwango kidogo.  Kwa jumla ni kwamba hili si suala la uhamiaji haramu bali ni la biashara haramu ya kusafirisha binadamu.
Ndugu Wananchi;
Kufuatia vyombo vyetu vya usalama kuwa makini na watu wengi kukamatwa ndipo wasafirishaji walipobuni njia za kuwasafirisha kama mizigo.  Makontena, malori yaliyofunikwa nyuma na matenki ya mafuta na ya maji yamekuwa yanatumika kwa ajili hiyo.  Usafiri wa aina hiyo ndiyo uliosababisha vifo vilivyotokea Dodoma tarehe 26 Juni, 2012 na vya watu 21 vilivyotokea mwezi Desemba, 2011 Mkoani Morogoro, na vile vya watu 12 vilivyotokea katika matukio mawili ya Mkoa wa Mbeya, mwezi Mei, 2012.
Ndugu Wananchi;
Tarehe 27 Juni, 2012 nilikutana na wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama nchini kuzungumzia tukio la Chitego na suala zima la biashara hii haramu na hasa mbinu mpya inayotumiwa na wasafarishaji.  Nilitoa pongezi kwa vyombo vya dola kwa kazi nzuri waifanyayo kudhibiti shughuli za biashara hii haramu hapa nchini.  Tulielewana kuwa waendelee kuimarisha udhibiti huo kwa lengo la kukomesha kabisa biashara hii.
 Niliagiza pia kwamba kikundi kazi nilichokiunda mwaka 2006 kushughulikia ujambazi sasa kielekeze sehemu ya nguvu zake kukabili tatizo hili. Aidha, kwa pamoja tulikubaliana kuwa nchi yetu ishirikiane na wenzetu wa Ethiopia, Kenya, Malawi, Msumbiji na Afrika ya Kusini kutambua mawakala na kuwabana kwa mujibu wa sheria.  Tayari nimeshaanza kufanya mawasiliano na baadhi ya Wakuu wa Nchi hizo kuhusu ushirikiano huo.  Nashukuru wote wameafiki nchi zetu zishirikiane kwa pamoja kuvunja mtandao huu mchafu na kutokomeza biashara hii haramu na inayodhalilisha utu wa mwanadamu.
Ndugu Wananchi;
Napenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru wenzetu, wakazi wa vijiji vya Chitego na Mkoka kwa kazi nzuri walioifanya. Kwa kweli, wenzetu wameonesha uzalendo wa hali ya juu kwa kutoa taarifa mapema juu ya jambo lenyewe, lakini pia wameonesha utu kwa kuwajali wageni waliokumbwa na janga hili. Naushukuru pia uongozi wa Mkoa wa Dodoma na Morogoro ikiwa ni pamoja na vyombo vya ulinzi  na usalama kwa kulishughulikia tatizo hilo kwa umakini mkubwa.   Nimefurahishwa sana na ushirikiano ulioonyeshwa na vyombo na taasisi mbalimbali za Serikali katika kushughulikia suala hili.
Mgomo wa Madaktari
Ndugu Wananchi;
          Jambo la pili ni kuhusu mgomo wa Madaktari unaoendelea nchini hivi sasa.  Nilipozungumza na Wazee wa Dar es Salaam katika Ukumbi wa Diamond Jubilee tarehe 12 Machi, 2012, kuhusu mgomo wa Madaktari uliokuwa unaendelea wakati ule pamoja na kuelezea chimbuko la mgomo na hatua iliyokuwa imefikiwa, nilielezea mazungumzo yangu na viongozi wa Chama cha Madakari wakiwemo pia viongozi wa Jumuiya ya Madaktari.  Nilitoa taarifa kuwa tumeelewana kuwa watasitisha mgomo na watarudi kwenye meza ya majadiliano na Serikali.  Siku ile pia nilielezea matumaini yangu kuwa mgomo ule utakuwa wa mwisho katika nchi yetu.  Bahati mbaya matumaini yangu hayo hayakuwa na hivi sasa tunashuhudia tena wagonjwa wakiteseka, kuhangaika na wengine kufa kwa sababu ya kukosa huduma wanazostahili kwa vile madaktari wao wamegoma tena.
Ndugu Wananchi;
Kama walivyoniahidi, madaktari waliacha kugoma na viongozi wao walirudi kwenye mazungumzo na Serikali.  Kama ilivyoagizwa na Mahakama Kuu, Kitengo cha Kazi tarehe 8 Machi, 2012, kwa mujibu wa Sheria ya Mahusiano Kazini, Namba 6 ya mwaka 2004.   Chama cha Madaktari na Serikali walifika katika Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (Commission for Mediation and Arbitration) kwa ajili ya majadiliano.  Kwa pamoja na kwa ridhaa yao wote, pande hizo mbili ziliiomba Tume hiyo iwape fursa ya kuzungumza wao wenyewe na wakimaliza mazungumzo wataenda kusajili makubaliano yao.  Tume ikawakubalia.  Ni vizuri ikakumbukwa kuwa siku ile ya tarehe 8 Machi, 2012 Mahakama Kuu Kitengo cha Kazi, ilitoa zuio la mgomo pamoja na kuagiza kuwepo mazungumzo baina ya pande mbili.
Ndugu Wananchi;
Kati ya tarehe 10 Aprili, 2012 na tarehe 30 Mei, 2012, vilifanyika vikao sita vya majadiliano kati ya Serikali na Chama cha Madaktari.  Katika mazungumzo hayo hoja au madai 12 ya madaktari yalizungumzwa.  Mambo hayo ni haya yafuatayo:
  1. Posho ya kuitwa kazini (on call allowance) iwe asilimia 10 ya mshahara.
  2. Posho ya kufanya kazi katika mazingira hatarishi (Risk allowance) iwe asilimia 30 ya mshahara.
  3. Madaktari wapatiwe nyumba grade A au posho ya makazi ambayo iwe asilimia 30 ya mshahara.
  4. Posho ya kufanya kazi katika mazingira magumu iwe asilimia 40 ya mshahara.
  5. Madaktari walipwe posho ya usafiri ya asilimia 10 ya mshahara au wakopeshwe magari.
  6. Madaktari wanaoanza kazi walipwe mshahara wa shilingi 3,500,00/= kwa mwezi.
  7. Madaktari wapatiwe Green Card za Bima ya afya.
  8. Hatua za kinidhamu zichukuliwe dhidi ya Watendaji Wakuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii.
  9. Viongozi wa Kisiasa kulazimisha kupewa rufaa nje.
  10. Madaktari waliofukuzwa warudishwe kazini.
  11. Huduma za afya ziboreshwe nchini.
  12. Posho ya uchunguzi wa maiti iongezwe.

Ndugu Wananchi;
          Katika mambo hayo 12 pande zote mbili zilifikia muafaka na kukubaliana wa pamoja kwa mambo saba.  La kwanza, ni kuhusu usafiri wa kwenda na kurudi kazini.  Serikali ilieleza kuwa upo utaratibu kwa mujibu wa Waraka wa Utumishi wa Serikali Na. 3 wa mwaka 2011 wa kuwakopesha wafanyakazi wa Serikali fedha za kununulia magari au pikipiki, samani na matengenezo ya magari.  Ilikubaliwa kuwa madaktari waitumie fursa hiyo.
          Jambo la pili, ni kuhusu madaktari kupatiwa Green Card za Bima ya Afya.  Jambo hili lilikubaliwa na Serikali na Wizara ya Afya imekwishachukua hatua za utekelezaji wake.
          Jambo la tatu, ni kuhusu hatua za kinidhamu kuchukuliwa dhidi ya Watendaji Wakuu wa Wizara ya Afya.  Kwa pamoja walikubaliana kuwa suala hilo liko nje ya mamlaka ya Kamati yao ya pamoja, waziachie mamlaka husika za uteuzi.  Uongozi wa juu wa Wizara umebadilishwa na sasa kuna uongozi mpya.  Lakini, jambo la kustaajanisha hata Waziri mpya wa Afya alipowataka waonane kuzungumzia hoja walikataa kumuona.  Kwanza walisema hawaoni sababu kwa vile wameyazungumza na Kamati yake kwa miezi mitatu bila ya mafanikio
          Jambo la nne walilokubaliana ni kuhusu viongozi kulazimisha kupewa rufaa ya kutibiwa nje.  Walikubaliana mambo mawili.  Kwanza, kwamba maelekezo ya Waziri Mkuu, Mhe. Mizengo Pinda kuwa madaktari wazingatie maadili ya kazi zao na kukataa kutoa rufaa kwa mtu asiyestahili awe kiongozi au asiwe kiongozi. Pili, walikubaliana kuwa hospitali zilizopo ziboreshwe ili viongozi watibiwe hapa nchini.  Ukweli ni kwamba kufanya hivyo ndiyo sera ya Serikali.  Nililieleza hili mwezi Desemba 30, 2005 katika hotuba yangu ya kuzindua Bunge baada ya kuchaguliwa kwa mara ya kwanza kuongoza nchi yetu.
Tumeiongeza sana bajeti ya sekta ya afya kutoka shilingi bilioni 300 2005/2006 hadi shilingi trilioni 1.2 mwaka 2011/12 na imekuwa ya tatu baada ya miundombinu na elimu.  Tumeziimarisha hospitali za Mikoa kwa vifaa tiba na wataalamu wa afya.  Kazi inaendelea katika hospitali za Wilaya. Tumewekeza katika Hospitali ya Muhimbili.  Hospitali hiyo ilivyo leo sivyo ilivyokuwa miaka sita nyuma.  Na kazi inaendelea hasa katika maeneo ambayo tunapeleka wagonjwa nje.  Matunda yake yanaanza kuonekana kwa upande wa figo, moyo, kinywa na mipango inaendelea kwa upande wa ubongo na mishipa ya fahamu.  Tunaendelea kuimarisha mafunzo ya  madaktari na madaktari bingwa, yote kwa nia hiyo hiyo.  Hivi sasa Chuo Kikuu cha Sayansi ya Tiba,Muhimbili kinachukua wanafunzi wengi zaidi ya ilivyokuwa siku za nyuma na makazi mapya ya chuo yanaendelea kuandaliwa ili kuchukua wanafunzi wengi zaid.    Mwaka 2005 tulikuwa na madaktari bingwa 46 mwaka huu tunao 520.
Ndugu Wananchi;
          Jambo la tano ambalo pande zote mbili zilikubaliana ni kuhusu madaktari waliofukuzwa.  Hawa ni wale Interns waliokuwa wamerudishwa Wizarani kutoka Muhimbili na kupangiwa hospitali za Temeke, Ilala, Mwananyamala na Lugalo.  Hili ni jambo ambalo lilikuwa limemalizika kitambo na wote walikuwa wamerudi Muhimbili.
          Jambo la sita ni kuhusu mapendekezo mbalimbali yaliyotolewa na madaktari kuhusu kuboresha huduma ya afya.  Mapendekezo hayo yalihusu kutathmini sera na mpango wa afya ya msingi, bajeti ya afya kuwa asilimia 15 ya bajeti ya Serikali, kuwepo na utaratibu mzuri wa kuajiri madaktari na kuboresha viwango vya ubora wa madaktari na kadhalika.  Serikali imeyaafiki mapendekezo hayo na yatafanyiwa kazi.
          Jambo la saba, ambalo pande zote walilokubaliana ni kuhusu kuongeza posho ya uchunguzi wa maiti.  Hili ni jambo jipya halikuwepo mwazoni.  Hata hivyo, Serikali imelikubali na posho hiyo imeongezwa kutoka shilingi 10,000/= hadi kufikia shilingi 100,000/= kwa daktari na shilingi 50,000/= kwa wasaidizi wake.
Ndugu Wananchi;
          Kuna masuala matatu ambayo yamekuwa na muafaka kwa kiasi fulani na kutoafikiana kwa baadhi ya mambo.  La kwanza ni suala la kufanya kazi katika mazingira hatarishi.  Serikali imekubali hoja ya kuchukua hatua ya kuwalinda madaktari wanaofanya kazi katika mazingira hatarishi.  Serikali iliwaeleza kuwa watumishi wa kada zote za afya watapatiwa chanjo dhidi ya maambukizi ya Hepatitis B na fedha zimetengwa katika bajeti ya 2012/13.
Aidha, Serikali imeeleza dhamira ya kurudisha posho ya mazingira hatarishi kwa watumishi wa umma wanaostahili.  Utekelezaji wake utafanyika baada ya uchambuzi wa kina wa kubainisha mazingira hatarishi ni yepi, viwango stahiki viwe vipi na nani hasa wahusike.  Madaktari wamekataa hili la kufanya uchambuzi, wanataka kiwango kiwe kama wanavyotaka wao, yaani asilimia 30 ya mshahara na kianze mara moja.
          Jambo la pili ambalo wamekubaliana nusu nusu ni kuhusu nyumba za kuishi.  Serikali imekiri wajibu wake wa kuwapatia madakari nyumba za kuishi.  Aidha, imeeleza mpango ulioanza wa kujenga nyumba 700 za madaktari kote nchini na kwamba hivi sasa ujenzi wa nyumba 90 unaendelea, 50 katika mkoa wa Mtwara na 40 katika mkoa wa Rukwa.
 Kwa maeneo ambayo madaktari wanalipwa posho ya pango Serikali imesema waajiri wataendelea kufanya hivyo kwa mujibu wa taratibu zilizopo kwa watumishi wa umma wenye stahili ya kupewa nyumba.  Jambo hilo limekataliwa na Madakari na kutaka lazima walipwe asilimia 30 ya mshahara kama posho ya nyumba.  Serikali kwa upande wake imeona vigumu kufanya hivyo na kuwasihi wakubali wanayotendewa wafanyakazi wengine wote wa umma.
          Jambo lingine ambalo lilikuwa na makubaliano ya nusu nusu ni kuhusu posho ya kufanya kazi katika mazingira magumu.  Pande zote mbili ziliafikiana kuwa yapo baadhi ya maeneo nchini yanayo mazingira magumu kwa watumishi wa umma  hivyo hatua zichukuliwe kuwasaidia watumishi hao. Serikali imekubali wajibu wa kuweka utaratibu wa kuboresha maisha ya watumishi katika maeneo hayo.  Kwa ajili hiyo, Serikali itatoa mwongozo kwa mamlaka za ajira kuhusu namna ya kuwasaidia watumishi hao kupunguza makali ya maisha katika kila eneo badala ya kutegemea posho peke yake.
  Kuhusu posho, Serikali imeeleza kuafiki kuwepo posho ya aina hiyo ila itatekelezwa baada ya kufanya uchambuzi wa kuainisha mazingira husika, kutambua watumishi waliopo na gharama zake.
          Madaktari hawajakubali kusubiri zoezi la uchambuzi lifanyike, wanataka Serikali ilipe posho hiyo sasa.  Tofauti hapa si posho hiyo kuwepo, bali ni rai ya Serikali ya kubaini maeneo yenyewe na kupanga aina ya hatua na viwango vya posho kulingana na mazingira halisi ya maeneo.  Madaktari hawaoni haja ya kufanya hayo.
Ndugu Wananchi;
          Mambo mawili hayakuwa na muafaka kabisa kati ya pande zetu mbili.  Jambo la kwanza ni posho ya kuitwa kazini (on call allowance).  Kwanza sina budi kueleza kuwa Serikali imekubali kuongeza posho hiyo.  Tangu Februari, 2012 posho iliongezwa kutoka shilingi 10,000/= hadi shilingi 25,000/= kwa daktari bingwa (Specialist), shilingi 20,000/= kwa dakari mwenye usajili wa kudumu (Registrars) na shilingi 15,000/= kwa madaktari waliohitimu ambao wapo katika kipindi cha mafunzo kazini (Interns).  Viwango hivyo vya posho vinatumika hivi sasa.
  Madaktari kwa upande wao hawakukubali uamuzi huo wa Serikali na kusisitiza walipwe asilimia 10 ya mshahara.  Ugumu wa kukubali pendekezo la madakari ni kuwa sharti la malipo haya ni mtu kuitwa kazini.  Ukitaka ilipwe kiwango cha mshahara ina maana kuwa hata kama daktari hakupangwa kuitwa au alipangwa na hakutokea aendelee kulipwa.  Hili haliwezi kuwa sahihi kufanya.  Linaweza kuwafanya baadhi ya madaktari kutokutimiza wajibu wao kwa vile wana hakika mwisho wa mwezi malipo yako pale pale.
Ndugu Wananchi;
Jambo la pili ambalo muafaka haukufikiwa baina ya Serikali na madaktari ni kuhusu mshahara wa kuanzia kazi wa daktari.  Madaktari wanataka uwe shilingi 3,500,000/= wakati Serikali inasema kiasi hicho hatukiwezi.  Serikali imeeleza utayari wake wa kuongeza mshahara kwa kati ya asilimia 15 mpaka 20 kama ambavyo itafanya kwa watumishi wote wa umma katika mwaka huu wa fedha.  Kwa kiwango cha sasa cha mshahara wao, daktari ataanzia kati ya shilingi 1,100,000/= na 1,200,000/= kutegemea kiwango kipi hatimaye kitaamuliwa.  Madaktari wamekataa katakata na wameng’ang’ania shilingi 3,500,000/=.
Ndugu Wananchi;
Huo ndiyo mlolongo wa mambo yaliyozungumzwa na pande zote mbili na matokeo ya mazungumzo yenyewe.  Katika kikao cha sita kilichofanyika tarehe 30 Mei, 2012, upande wa Chama cha Madaktari ulisema kuwa kwa vile hoja ya nyongeza ya mshahara haina mabadiliko hawakuona haja ya kuendelea na majadiliano mpaka watakapowasiliana na wenzao.  Waliahidi kutoa taarifa ndani ya wiki mbili.  Tarehe 12 Juni, 2012, Rais wa MAT aliandika barua kwa Katibu Mkuu Utumishi ambaye ndiye kiongozi wa majadiliano kwa upande wa Serikali, kuwa Madaktari wameikataa taarifa na ufafanuzi waliopewa kutoka Serikalini kwa ujumla wake.
Ndugu Wananchi;
 Baada ya majibu yale ya madaktari, tarehe 19 Juni, 2012, Serikali na Madaktari walikwenda kwa Msuluhishi (CMA) kutoa taarifa kuwa mgogoro umekosa usuluhishi kama sheria inavyotaka.  Kwa pamoja pande zote mbili zilikubaliana suala hilo lifikishwe Mahakama Kuu Kitengo cha Kazi.  Wakati pande zote zinasuburi mgogoro huu kufikishwa ngazi hiyo ya juu, upande wa Madaktari ukatangaza kuwepo kwa mgomo kuanzia saa sita ya usiku tarehe 23 Juni, 2012.  Hatua hiyo haikustahili kwani suala lenyewe halijafika mwisho wa kushughulikiwa kwa mujibu wa Sheria za Mahusiano ya Kazi nchini.
Ndugu Wananchi;
Tarehe 22 Juni, 2012, Mwanasheria Mkuu wa Serikali akaenda Mahakama Kuu Kitengo cha Kazi kulifikisha suala la tishio la mgomo na kuomba zuio la muda kufanywa.   Mahakama Kuu ilikubali ombi hilo na kuagiza kuwa mgomo usitishwe.  Juhudi za kumtafuta Rais wa MAT, Dkt. Namala Mkopi na viongozi wengine wa MAT hazikufanikiwa, Ofisi ya MAT ilikuwa imefungwa na simu zote za viongozi wa MAT zilikuwa zimezimwa.  Hatimaye tarehe 25 Juni, 2012, alipatikana na kupewa amri hiyo ya Mahakama.  Tarehe 26 Juni, 2012, Dkt. Mkopi alifika Mahakamani ambapo alikana kuwa yeye hahusiki na kuitisha huo mgomo lakini hakumtaja aliyehusika.  Pamoja na rai hiyo, Jaji alimuamuru Rais wa MAT akawatangazie wanachama wake kusitisha mgomo.   Dkt. Namala Mkopi hajafanya hivyo hadi leo na mgomo umekuwa unaendelea kinyume cha Sheria.
Ndugu Wananchi;
Wagonjwa wanateseka na wengine kupoteza maisha kwa mgomo huu usiokuwa halali kisheria ambao pia haustahili kuwepo hata kwa mujibu wa maadili ya udaktari.  Viongozi wa  MAT na wenzao wanawaingiza Madaktari katika mgogoro na Mahakama na waajiri wao isivyostahili.  Ni vyema viongozi wa Madaktari na madaktari wakatambua kuwa wanashiriki katika mgomo usiokuwa halali ambao pia kiongozi wao mkuu amekana Mahakamani kuwa hahusiki nao.  Madaktari lazima watambue pia kwamba ajira zao wanaziweka hatarini.  Mfanyakazi ana kinga ya kutofukuzwa kazi na mwajiri kwa kushiriki mgomo unaokubalika kisheria.  Huu siyo.  Watapoteza ajira, hawana pa kukimbilia, hawana cha kiwalinda.  Kwa madaktari interns, wanahatarisha maisha yao kwani hawatapata cheti cha kudumu wakishiriki mgomo usiokuwa halali.   Lazima watafakari sana kwa hayo wafanyayo.
Ndugu Wananchi;
          Napenda kurudia maneno niliyoyasema tarehe 12 Machi, 2012, kuwa kuboresha mishahara na maslahi ya wafanyakazi ni Sera ya Serikali yetu kwa maelekezo ya Ilani ya Chama Tawala (CCM).  Tumeitekeleza kwa vitendo sera hiyo, hata hivyo ni ukweli ulio wazi kuwa nia yangu njema tu pekee haitoshi, lazima uwezo wa kufanya hivyo uwepo.  Kwa kulingana na uwezo uliopo, tumeendelea kuboresha mishahara na maslahi ya wafanyakazi hatua kwa hatua tangu tuingie madarakani.  Tumefanya hivyo kwa jumla kwa wafanyakazi wote na kwa kada mbalimbali za watumishi wa umma.
Miongoni mwa wafanyakazi wa umma walionufaika na hatua hizo za Serikali ni madaktari na watumishi wa kada nyingine za huduma ya afya.  Tena nadiriki kusema madaktari tumewapa upendeleo mkubwa kuliko watumishi wengine wa umma.  Upendeleo upo kwenye mafunzo ambapo wanafunzi wa udaktari wanagharimiwa na Serikali kwa asilimia mia moja wakati wanafunzi wenzao wa taaluma nyingine hawako hivyo.
Ndugu Wananchi;
Mwaka 2004/2005, mshahara wa kuanzia wa daktari ulikuwa shilingi 178,700/=, mwaka 2005/ 2006 tuliupandisha na kuwa shilingi 403,120/=. Tuliendelea kuupandisha mwaka hadi mwaka mpaka kufikia shilingi 957,700/= wanazolipwa sasa.  Kiasi hicho ni mara mbili ya mishahara ya watumishi wa taaluma nyingine wenye shahada ya kwanza wanaoanza kazi ambao kwa wastani hupata shilingi 446,100/=.
Tunafanya hivyo kwa kutambua na kuthamini nafasi maalum ya madaktari katika jamii na ukweli kwamba bado tunayo safari ndefu ya kuziba pengo la madaktari nchini.  Lakini inaonekana juhudi zetu zote hizo hazithaminiwi.
Ndugu Wananchi;
Sina budi kusisitiza  kwamba tunapofanya hivyo tunaongozwa na uwezo tulio nao wa kulipa.   Kwa sasa hatuwezi kuwaahidi kuwa tunao uwezo wa kuwalipa mshahara wa kuanzia wa shilingi 3,500,000/= na posho zote zile. Tukifanya hivyo malipo ya daktari anayeanza kazi yatakuwa shilingi 7,700,000/=.  Kwa hakika kiasi hicho hatutakiweza. Si vyema kutoa ahadi hewa kwa watu tunaowaheshimu na kuwathamini kama walivyo madaktari.
Kutokana na ukweli huo basi kama daktari anayeona kuwa hawezi kufanya kazi Serikalini bila ya kulipwa mshahara huo awe huru kuacha kazi na kwenda kwa muajiri anayeweza kumlipa kiasi hicho.  Nasi tutamtakia kila la heri.  Hana sababu ya kugoma ili ashinikize kulipwa mshahara huo. Asisumbuke, hatalipwa mshahara huo.  Isitoshe, hana sababu ya kuendelea kuwa na mgogoro na mwajiri ambaye hana uwezo wa kumlipa anachokitaka.  Huna sababu ya kumpa usumbufu mwajiri wa kukuandikia barua ya kujieleza au kukuachisha kazi.  Kwa nini upate usumbufu wa kupata barua hizo na kuzijibu. Kwa nini upate usumbufu wa kuachishwa kazi na kutakiwa kuondoka kwenye nyumba ya Serikali ndani ya saa 24.  Jiepushe na yote hayo kwa kujiondoa mwenyewe.  Usipofanya hivyo, mwajiri anakuwa hana jinsi bali kukuondoa kazini maana unakwenda kinyume na sheria za kazi na maadili ya kazi ya udaktari.
  Mamlaka za ajira zimeanza kuchukua hatua hizo na wataendelea kufanya hivyo kwa wote wanaoendelea kugoma.   Najua baada ya hatua hizo kuchukuliwa kuna manun’guniko ya kuonewa. Hivyo, mlitegemea mwajiri afanyeje? Ni bora kufanya hivyo ili ajue hana daktari aweze kufanya utaratibu wa kuziba hilo pengo na huyo ajae awe na mahali pa kuishi. Vinginevyo atakuwa anajidanganya kuwa anae daktari ambae hayupo kazini na wala hataki kufanya kazi.
Ndugu Wananchi;
Napenda kuwathibitishia kwamba dhamira ya Serikali ya kuboresha maslahi ya watumishi wa umma wakiwemo  madaktari iko wazi.  Tumekuwa tunafanya hivyo, na tutaendelea kufanya hivyo kulingana na uwezo wa kibajeti.  Ni vyema watumishi wa umma wakatambua kuwa hatuwezi kutumia fedha zote au kiasi kikubwa mno cha pesa za umma kulipana mishahara.  Tukifanya hivyo, Serikali itashindwa kutoa huduma muhimu kwa wananchi ambao ndiyo wengi na wanastahili kuhudumiwa.  Hata hizo huduma za afya tunazosema ni duni tuziboreshe, hatutaweza kuziboresha kama tutatumia sehemu kubwa ya pesa za Serikali kuwalipa mishahara wafanyakazi.
Hivi sasa matumizi ya mishahara ni asilimia 48 ya bajeti ya Serikali.  Kiwango hicho ni kikubwa mno.  Uwiano mzuri ni kuwa na matumizi ya mishahara yasiyozidi asilimia 35 ya bajeti na asilimia 65 zitumike kugharimia huduma na shughuli nyingine za maendeleo ya wananchi na taifa.  Sisi tumezidi kwa asilimia 13.  Hivyo, hatuna budi tukubali kujinyima kwa manufaa ya walio wengi.
Suala la Dkt. Steven Ulimboka
Ndugu Wananchi;
Kabla ya kumaliza hotuba yangu, napenda kuungana na Watanzania wenzangu wote kuelezea masikitiko yangu makubwa na kuhuzunishwa kwangu na kitendo cha kinyama alichofanyiwa Dkt. Steven Ulimboka usiku wa tarehe 26 Juni, 2012. Kitendo hicho ni kinyume kabisa na mila na desturi zetu. Watanzania hatujayazoea mambo hayo. Nimeelekeza vyombo vyetu vya ulinzi na usalama kufanya uchunguzi wa kina ili ukweli ujulikane.  Nimesema kuwa ningependa ukweli huo ujulikane mapema ili tuondoe wingu baya la kutiliana shaka na kulaumiana kunakoendelea hivi sasa.
Natambua kuwa Serikali nayo inatajwa katika orodha ya wanaotiliwa shaka.  Mimi nimeshangazwa sana na hisia hizo kwani siioni sababu ya Serikali kufanya hivyo.  Dkt. Ulimboka alikuwa mmoja wa kiungo muhimu katika mazungumzo baina ya Serikali na Madkatari.  Ni kweli kwamba yeye si mtumishi wa Serikali, hivyo hakustahili kuwa sehemu ya majadiliano haya.  Kulikuwa na rai ya kutaka asiwepo, lakini nilisema wamuache maadam Madaktari wanamuamini kuwa anaweza kuwasemea vizuri zaidi kuliko wao wenyewe walioajiriwa na Serikali.
Ndugu Wananchi;
Kama nilivyoeleza, mazungumzo yalienda vizuri na mafanikio makubwa yamepatikana.  Yapo maeneo machache na hasa eneo la mshahara ambalo hatukuweza kukubaliana.  Hapo tulipofikia si pabaya na tulikubaliana sote kurudi kwenye mkondo wa Sheria kusaidiwa.  Kwa nini Serikali imdhuru Dkt. Ulimboka? Na, kuhusu mgomo, Mahakama Kuu imekwishatoa amri ya kusitisha mgomo.  Anayekaidi amri ya Mahakama ananunua ugomvi na mhimili huo wa dola ambao wenyewe una mamlaka ya kumtia adabu mtu huyo.  Hivi baada ya kufika hapo Serikali iwe na ugomvi na Dkt. Steven Ulimboka kwa sababu ipi na jambo lipi hata iamue kumdhuru?  Kama kuna mtu wa Serikali kafanya, itakuwa kwa sababu zake binafsi na siyo za Serikali au kwa kutumwa na Serikali.
Ndugu Wananchi;  
Kwa niaba yangu na kwa niaba ya Serikali natoa mkono wa pole kwa Dkt. Steven Ulimboka na kumuombea apone haraka ili aungane na familia yake na Watanzania wenzake katika ujenzi wa taifa.  Kwa namna ya pekee namshukuru na kumpongeza Bwana Juma Mgaza, kwa moyo wake wa huruma na upendo na kwa hatua alizochukua za kumsaidia Dkt. Ulimboka.
Naomba kumaliza kwa kuwasihi madaktari kuacha mgomo na kurejea kazini.  Watanzania wenzenu wanateseka na kupoteza maisha.  Muwe na moyo wa huruma na upendo na msaada kwa wagonjwa kama kiapo chenu kinavyowataka.
Mungu Ibariki Afrika!
Mungu Ibariki Tanzania!
Asanteni kwa Kunisikiliza.